Tuesday, May 28, 2013

URUSI KUISAIDIA SYRIA KWA SILAHA, YAPINGANA NA E.U.

Rais wa Urusi Dimitry Medvedev
MOSCOW-URUSI,
Serikali ya Urusi imekosoa vikali uamuzi uliofikiwa na viongozi wa Umoja wa Ulaya kuhusu kukataa kuongeza muda wa vikwazo vya silaha dhidi ya waasi wa Syria na kuongeza kuwa kufanya hivyo kutachochea machafuko zaidi nchini Syria.

Kauli ya Urusi inatolewa ikiwa zimepita saa chache toka mawaziri wa mambo ya kigeni wa Umoja wa Ulaya EU wamalize mkutano wao mjini Brussels Ubelgiji na kukubaliana kutoongeza muda wa vikwazo vya silaha kwa waasi, hatua inayoruhusu waasi hao kuwezeshwa kwa silaha.

Naibu waziri wa mambo ya kigeni wa Urusi, Sergei Ryabkov amesema kuwa nchi yake imesikitishwa na hatua ya Umoja wa Ulaya kuwaondolea vikwazo vya silaha waasi na kwamba kufanya hivyo kunatoa mwanya hata kwa makundi mengine ya kigaid kuweza kupata silaha kutekeleza uasi zaidi nchini Syria.

Urusi inatoa kauli hyo wakati huu ikijiandaa kupeleka silaha zaidi kwa Serikali ya rais Assad aina ya S-300 silaha zinazoweza kutumika kudungua ndege za kijeshi iwapo mataifa ya magharibi yataamua kuivamia Syria kijeshi.

Hatua hiyo ya Urusi inaendelea kuibusha mgawanyiko zaidi kati ya mataifa ya magharibi ambazo yameiweka vikwazo nchi ya Syria kupata silaha.

Serikali ya Urusi inasema kuwa mpango huo wa kuisaidia Syria kwa zana za kijeshi ni mkataba uliotiwa saini kati ya nchi hizo mbili miaka miwili iliyopita na kwamba ni lazima watekeleze azma yao.

Mtafaruku huu mpya unaibuka wakati huu ambapo Urusi na Marekani zimeandaa mkutano wa kimataifa mjini Geneva Uswis, mkutano utakaowakutanisha upande wa waasi na Serikali kwa mara ya kwanza.

Katika hatua nyingine upinzani nchini Syria umeendelea kugawanyika kuhusu uundwaji wa Serikali yao huku makundi zaidi yakiibuka yakiwa na mtazamo tofauti kuhusu vita vya Syria hali inayofanya vita kuwa ngumu zaidi kwa upande wa waasi.

No comments:

Post a Comment