Sunday, April 28, 2013

Mambo matatu aliyohojiwa Lema ndani ya masaa matatu na Polisi

ARUSHA-TANZANIA,Kushikiliwa kwa Mbunge wa Arusha Mjini (Chadema), Godbless Lema kumeendelea kuibua sokomoko baina ya polisi kwa upande mmoja na wafuasi wa Chadema na familia yake kwa upande mwingine.
\Lema aliyekamatwa usiku wa manane kuamkia Ijumaa wiki hii, alihojiwa kwa saa tatu mfululizo katika Kituo Kikuu cha Polisi, Arusha lakini alinyimwa dhamana kwa maelezo kwamba kuachiwa kwake kungehatarisha amani.
Akizungumza na gazeti hili kabla ya kujisalimisha kwa askari hao usiku huo wa kuamkia juzi, Lema alithibitisha kuwapo kwa polisi nje ya nyumba yake:
“Wapo nje ya nyumba yangu, wanatishia kupiga mabomu kama nisipotoka nje, lakini wanajadiliana na walinzi wangu na mimi nimewataka wanipe hati ya kunikamata,”alisema.
Wakili wa Lema, Humphrey Mtui alisema mahojiano ya mteja wake na polisi yalidumu kwa zaidi ya saa tatu kuanzia saa 7:50 mchana hadi saa 11:15 jioni, na kwamba walitaka ufafanuzi kwenye hoja tatu walizodai kwamba zilijengwa kwenye kauli alizotoa Lema wakati alipokuwa akizungumza na wanafunzi wa Taasisi ya Uhasibu Arusha (IAA).
Maneno hayo yanayotafsiriwa na polisi kuwa ni uchochezi ni pamoja na “Dhambi mbaya na kubwa kuliko zote duniani ni woga” na “Nimepata taarifa kuwa ndani ya dakika 15 Mkuu wa Mkoa atafika, asipofika ndani ya muda huo nitawaongoza kwenda kudai haki yenu ya msingi ya kupatiwa ulinzi.”
Kauli nyingine ni “Hawa ndio viongozi wetu (akimaanisha mkuu wa mkoa), tunaowategemea wanakuja kwenye matatizo wakijivuta utafikiri wanakwenda kwenye send-off.”()
Lema anadaiwa kutamka maneno hayo baada ya Mulongo kugoma kuzungumza na wanafunzi kisha kurejea ndani ya gari akitaka viwepo vipaza sauti, kitendo kilichowafanya wanafunzi kuanza kumzomea kabla polisi kuanza kulipua mabomu ya machozi na kumwondoa eneo la tukio mkuu huyo wa mkoa.
Lema na Mulongo wote walikwenda IAA kutokana na tukio la kuuawa kwa kuchomwa kisu kwa aliyekuwa mwanafunzi wa taasisi hiyo, Henry Kago.
Baada ya vurugu hizo Mulungo alimtuhumu Lema kuandaa mazingira ya yeye kuzomewa .
Wakati hayo yakiendelea, askari katika kituo anakoshikiliwa Lema jana asubuhi walivutana vikali na ndugu wa mbunge huyo pamoja na uongozi wa Chadema Mkoa wa Arusha baada ya kumpa dakika moja kunywa chai aliyoletewa na kukataa asipewe dawa ya meno kutoka kwa mkewe, Neema.
Habari ambazo gazeti hili lilizipata zinasema kutokana na hali hiyo, uongozi wa Chadema ulilazimika kumtuma wakili wa Lema, Method Kimomogoro kwenda Kituo cha Kati cha Polisi Arusha kujua sababu za polisi kufanya hivyo. (MWANANCHI)

Saturday, April 20, 2013

AZAM YABANWA NA AS FAR-ZATOKA SULUHU.

Azam FC playersDAR ES SALAAM-TANZANIA,Timu ya Azam Fc naAS FAR Rabaat ya Morocco, leo zimetoka suluhu katika mchezo wa kwanza wa hatua ya pili kombe la shirikisho la mpira wa miguu Afrika, uliochezwa katika uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam.

Katika mchezo huo azam fc iliwabidi wafanye mabadiliko ya mapema kwa kumpumzisha beki toka Kenya Jackson Atudo na nafasi yake kuchukuliwa na Lukson Kakolaki baada ya Atudo kuumia.
Katika dakika za mwanzo azam walichezea mpira katika eneo lao zaidi na kukaribisha mashambulizi ambayo yaliishia katika safu ya ulinzi ya azam fc iliyokuwa inaongoza na kipa Mwadini Ally.

Azam fc walifanya mashambulizi kadhaa katika lango la AS FAR katika kipindi hicho cha kwanza na kushindwa kuziona nyavu za wapinzani na kupelekea mpira kwenda mapumziko wakiwa suluhu.
Kipindi cha pili azam fc walizidisha masgambulizi katika lango la AS FAR, lakini uimara wa kipa wa waarabu hao walipelekea washamauliaji wa azam kushindwa kuingiza mpira kwenye nyavu za AS FAR.

Kipre Tchetche aliyepoteza nafasi mbili katika mchezo huo aligongesha mpira kwenye mwamba mara mbili katika dakika ya 53 na dakika za nyongeza.
Kocha wa azam fc Stewart Hall alifanya mabadiliko yaliyompeleka benchi Khamis Mcha aliyepoteza nafasi moja ya kuipatia goli azam fc na nafasi yake kuchukuliwa na Gaudence Mwaikimba, mabadiliko yaliyoshindwa kubadili matokeo na mchezo kwisha kwa sare ya bila kufungana.''

Azam na AS FAR wanataraji kurejeaana wiki mbili zijazo katika nchi ya Moroco ambapo azam wataitaji sare ya magoli ama washinde ili watinge katika hatua inayo fuata.

Friday, April 19, 2013

MUSHARAF AKAMATWA TENA.




ISLAMABAD-PAKISTAN,
Polisi nchini Pakistan wamemkamata rais wa zamani wa nchi hiyo Pervez Musharraf, kutokana na agizo la Mahakama siku ya Alhamisi.

Hatua ya kukamatwa kwa Musharraf ilitolewa na Mahakama hiyo kutokana na uamuzi wake wa kuagiza kifungo cha nyumbani kwa Majaji nchini humo mwaka 2007 akiwemo Jaji Mkuu.

Musharraf, alikamatwa nyumbani kwake nje kidogo ya mji wa Islamabad siku ya Ijumaa na kufikishwa Mahakamani huku serikali ikisema nyumba yake itakuwa jela kwa mujibu wa sheria ya nchi hiyo.

Kiongozi huyo wa zamani wa kijeshi ameonekana siku ya Ijumaa akisindikizwa na polisi Mahakamani na tayari anazuiliwa rumande kwa siku mbili kabla ya kupewa kifungo cha nyumbani.

Hii ni ndio mara ya kwanza kwa Mahakama nchini humo kutoa agizo la kukamatwa kwa kiongozi wa zamani wa nchi hiyo ambaye pia alikuwa Mkuu wa Majeshi.

Wakati uo huo, Mahakama mjini Islamabad imeanza kusikiliza kesi ya uhaini dhidi ya Musharraf kwa kuagiza kuwepo kwa sheria ya hatari nchini humo mwaka 2007 na ikiwa atapatikana na kosa atahukumiwa kifo au kufungwa maisha jela.

Kiongozi huyo wa zamani pia anatuhumiwa kupanga mauaji ya kiongozi wa upinzani Benazir Bhutto mwaka 2007.

Musharraf mwenye umri wa miaka 69 alikuwa rais wa kumi wa nchi hiyo kati ya mwaka 2001 hadi 2008 kabla ya kujiuzulu na kukimbilia ukimbozini jijini London nchini Uingereza.

Musharraf alirudi nyumbani mwezi uliopita kutoka Dubai alikokuwa anaishi, na kusema kuwa amerudi nyumbani ili kuikoa Pakistan hatua iliyokaatiliwa na tume ya uchaguzi nchini humo.

RAIS KIKWETE AONGOZA MAZISHI YA BI.KIDUDE




Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Maalim Seif Sharif akiweka udongo katika kaburi la Msanii mkongwe wa Taarab Tanzania, Fatma Baraka (Bi Kidude) katika makaburi ya Kitumba Wilaya Kati Mkoa wa Kusini Unguja.
Rais wa Jamhuri ya Muungano ya Tanzania ,Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete akiweka udongo kwenye kaburi la Msanii mkongwe wa Muziki wa Mwambao (Taarab) Tanzania,Marehemu Fatma Baraka (Bi Kidude) katika makaburi ya Kitumba Wilaya ya Kati Mkoa wa Kusini Unguja
.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein akiweka udongo katika kaburi la Msanii mkongwe wa Taarab Tanzania, Fatma Baraka (Bi Kidude) katika makaburi ya Kitumba Wilaya Kati Mkoa wa Kusini Unguja.

Msanii wa Muziki wa Kizazi Kipya,Nasibu Abdul Juma (Diamond) akiweka udongo kaburini wakati wa mazishi ya Msanii mkongwe wa Taarab Tanzania, Fatma Baraka (Bi Kidude) katika makaburi ya Kitumba Wilaya Kati Mkoa wa Kusini Unguja picha zote na Ikulu 

Thursday, April 18, 2013

MANCHESTER UNITED YAZIDIWA THAMANI NA REAL MADRID


LONDON-UINGEREZA,
Manchester United wameondolewa kwenye nafasi ya kwanza ya klabu yenye utajiri na thamani kubwa inayotolewa na jarida la Forbes.

United wamekuwa wakishika nafasi ya kwanza kila mwaka tangu Forbes walipoanza kutoa list ya vilabu vye thamani kubwa zaidi duniani mwaka 2004, lakini mwaka huu wameondolewa kileleni na Real Madrid - klabu ambayo iliitoa kwenye michuano ya champions league hive karibuni.

Barcelona wanashika nafasi ya tatu nyuma ya United, Arsenal wapo nafasi ya nne na mabingwa wa Bundesliga Bayern Munich wakikamilisha nafasi ya tano.

Real Madrid wanatajwa kuwa na thamani ya £2.15billion - na kwa namba hizo klabu hiyo ya Spain inakuwa ndio klabu ya michezo yenye thamani kubwa zaidi duniani - huku Manchester United wakiwa na thamani ya £2.07billion.

Kwa upande wa wachezaji wa soka, David Beckham bado anaongoza kwa utajiri akiwa ameingiza kiasi cha kati ya £33m - £29m ambazo zimetokana zaidi na mikataba ya kibiashara ya matangazo.

Staa wa Real Madrid Ronaldo ameingiza kiasi cha (£28.8m) akishika nafasi ya pili, wakati mwanasoka bora wa dunia Lionel Mess akishika nafasi ya 3 kwa kuingiza jumla ya £26m mwaka jana kwa kupitia mshahara na mikataba ya kibiashara.

HALI YATIBUKA BUNGENI-WABUNGE WATANO WATOLEWA NJE.



DODOMA-TANZANIA,
Wabunge watano wa Chadema jana walitimuliwa bungeni na kuamriwa kukaa nje ya Bunge kwa siku tano kutokana na vurugu zilizotokea jana usiku.


Wabunge hao ni Lissu, Hezekiah Wenje (Nyamagana), Highness Kiwia (Ilemela), Joseph Mbilinyi (Mbeya Mjini) Godbless Lema (Arusha Mjini) na Mchungaji Peter Msigwa (Iringa Mjini).


Chanzo za kufukuzwa kwao ni kuwazuia askari wa Bunge kumtoa nje Lissu ambaye alikuwa ameamriwa kutoka nje na Naibu Spika, Job Ndugai baada ya kuingilia hotuba ya Mbunge wa Iramba Mashariki, Mwigulu Nchemba.


Kutokana na tafrani hiyo, Nchemba hakuweza kuhitimisha hotuba yake hivyo Ndugai alilazimika kukatisha mkutano wa Bunge.Hata hivyo wakati akiahirisha mkutano huo, tayari wabunge hao walikuwa wameshatolewa nje baada ya askari kuongezwa.


Mapema Mbunge wa Kigoma Mjini (CCM), Peter Serukamba alitoa tusi zito la nguoni wakati wa hotuba ya Msemaji Mkuu wa Kambi ya Upinzani kwa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, licha ya Spika wa Bunge, Anne Makinda kupiga mkwara wa kuwashughulikia wabunge watakaorusha matusi.


Mbali na tukio hilo Lema naye alichafua hali ya hewa baada ya kuwatuhumu viongozi wa CCM akiwamo Rais Jakaya Kikwete kwa udini, madai ambayo Bunge limempa siku saba kuyathibitisha.


Lema aliituhumu CCM na Serikali yake chini ya Rais Kikwete kwa kushindwa kutatua mgogoro wa kidini na badala yake kuwa kama analikwepa tatizo. Alionya kuwa Taifa linapasuka kwa migogoro kutokana na viongozi wa Serikali kushindwa kulishughulikia.


Kauli iliwanyanyua vitini Waziri wa Nchi katika Ofisi ya Waziri Mkuu (Bunge na Uratibu na Sera), William Lukuvi na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema.
Lukuvi na Jaji Werema walisimama wakidai kuwa Lema alikuwa amemdhihaki Rais Kikwete kwa kauli zake za kumhusisha na masuala ya udini.


Hata hivyo, Mnadhimu Mkuu wa Upinzani, Lissu alisimama kumtetea Lema akidai hakuwa amemdhihaki Rais bali alikuwa amemkosoa kitu ambacho kanuni za Bunge zinaruhusu.


Lema aliruhusiwa kuendelea na hoja yake na ndipo akamtolea mfano Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Uhusiano na Uratibu), Steven Wassira wakati alipokwenda Mwanza kutatua mgogoro baina ya Wakristo na Waislamu kuhusu suala la kuchinja.


“Wassira akifahamu yeye ndiye, Waziri alikwenda Mwanza na kuwaacha viongozi wa dini za Kikristo na Kiislamu watatue wenyewe suala la kuchinja. Sasa alitaka diwani atatue mgogoro ule?”


Baada ya kumaliza kuchangia, Naibu Spika alitangaza kuwa Lema anatakiwa kuwasilisha katika muda wa siku saba uthibitisho kuwa Rais anahusika na tatizo la udini.(MWANANCHI)

Wednesday, April 17, 2013

AS FAR RABAT YA MOROCCO SASA KUTUA LEO.


DAR ES SALAAM-TANZANIA,
TIMU ya AS FAR Rabat ya Morocco itakayoikabili Azam kwenye mechi ya Kombe la Shirikisho inatua nchini leo (Aprili 17 mwaka huu) saa 7.30 mchana kwa ndege ya Qatar Airways.

Msafara wa timu hiyo wenye watu 28 kwa ajili ya mechi hiyo ya kwanza ya raundi ya pili itakayochezwa Jumamosi (Aprili 20 mwaka huu) saa 10 kamili jioni Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam utafikia hoteli ya Sapphire iliyoko maeneo ya Kariakoo.

Wakati Azam imetinga hatua hiyo baada ya kuitoa timu ya Barrack Young Controllers II ya Liberia kwa jumla ya mabao 2-1, AS FAR Rabat imeingia raundi hiyo moja kwa moja kutokana na nchi hiyo kufanya vizuri kwenye michuano ya klabu Afrika.

Timu nyingine ambazo zimeingia raundi hiyo moja kwa moja katika Kombe la Shirikisho kama ilivyo AS FAR Rabat ni Asec Mimosas ya Ivory Coast, Atletico Petroleos (Angola), C.S.S. (Tunisia), DC Motema Pembe (Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo- DRC), El Ahly Shandy (Sudan), Enppi (Misri), Heartland (Nigeria), Ismaily (Misri), Lobi Stars (Nigeria), U.S.M. Alger ya Algeria na Wydad Casablanca (Morocco).

Mwamuzi Emile Fred atakayesaidiwa na Steve Maire, Jean Ernesta na Jean Claude Labrossa wote kutoka Shelisheli ndiye atakayechezesha mechi hiyo. Kamishna ni Abbas Sendyowa kutoka Uganda. Waamuzi watawasili nchini kesho (Aprili 18 mwaka huu) jioni.

BI.KIDUDE AFARIKI DUNIA


ZANZIBAR-TANZANIA,
 Fatuma binti Baraka almaarufu kama Bi Kidude amefariki dunia mapema leo mjini Zanzibar.Bi kidude anayekadiriwa kuwa na umri wa miaka 116,alizaliwa katika kijiji cha Mfagimaringo huku zanzibar na alikuwa ni moja ya wakongwe wa muziki wa taarabu waliotamba tangu enzi za ujana mpaka uzee wake akijinyakulia tuzo mbali mbali zikiwemo Prestigious WOMEX award.

MUNGU AILAZE ROHO YAKE MAHALI PEMA PEPONI--AMEN!

Tuesday, April 16, 2013

MAREKANI YASHAMBULIWA KWA MABOMU-WATATU WAFARIKI NA MAMIA KUJERUHIWA

marathon



boston marathon explosions first responders

first responders boston marathon

first responders boston marathon

first responders boston marathon


BOSTON-MAREKANI,
Uchunguzi unaendelea kuwasaka watu waliohusika na mashambulizi mawili ya mabomu mjini Boston nchini Marekani wakati wa mbio ndefu na kusababisha vifo vya watu watatu na wengine zaidi ya mia moja kujeruhiwa.

Mashambulizi hayo yalitokea katika mstari wa kutamatisha mbio hizo, saa kadhaa baada ya washindi kupatikana katika mbio hizo ndefu wakati  wanariadha wengine wakiendelea kukimbia .
Shirika la FBI linaoongoza uchunguzi huo wa mashambulizi  hayo ambayo yanashukiwa kuwa wa kigaidi, uchunguzi ambao unalenga kufahamu kiini cha mashambulizi hayo na waliyoyatekeleza.
Polisi wanasema kuwa watu 17 wamejeruhiwa vibaya huku wengine wakikatwa miguu na mikono kutokana na uzito wa majereha yao.
Rais wa Marekani Barrack Obama amesema kuwa lazima waliotekeleza mashambulizi hayo wachukuliwe hatua za kisheria, huku Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki Moon akilaani tukio hilo.
Shambulizi la kwanza lilitokea saa mbili baada ya washindi kuvuka mstari wa mwisho huku polisi wakiwa na wakati mgumu kuwasaidia wale waliokumbwa na milipuko hiyo.
Polisi mjini Boston wametoa wito kwa wakaazi wa mji huo kuepuka mikusanyiko ya watu wakati huu ambao bado hali ya usalama si ya kuridhisha kutokana na mashambulizi hayo.
Miaka kumi iliyopita mashambulizi ya mabomu yalisababisha vifo vya zaidi ya watu elfu tatu  mjini New York,Washington DC  na Pennsylvania.

Saturday, April 13, 2013

YANGA NA OLJORO KIBARUANI LEO.

 
DAR ES SALAAM-TANZANIA,
VINARA wa Ligi Kuu soka Tanzania Bara, Yanga ya jijini Dar es Salaam leo wanatarajiwa kushuka Uwanja wa Taifa kuwakabili maafande JKT Oljoro katika mchezo unaotarajiwa kuwa mgumu.

Wakati Yanga wakikabiliana na JKT Oljoro, maafande wengine Tanzania Prisons watakuwa wakipigana kuepuka ukanda wa hatari kushuka daraja dhidi ya Ruvu Shooting kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine jijini Mbeya.

Yanga wenye pointi 49 watakuwa na kibarua kizito kuhakikisha wanashinda mechi hiyo ili kuzidisha tofauti ya pointi na Azam FC wanaokamata nafasi ya pili kwa pointi 46, baada ya juzi kuishinda African Lyon kwa mabao 3-1.
Awali Yanga na JKT Oljoro zilikuwa ziumane juzi kabla ya mechi hiyo kuahirishwa na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kwa ajili ya kutoa nafasi kuoneshwa ‘live’ na kituo cha runinga cha Super Sport.

Akizungumza na Tanzania Daima jijini Dar es Salaam jana, Daktari wa Yanga, Nassor Matuzya alisema vijana wao wako fiti na waliokuwa nje kutokana na majeraha hali zao zimetengemaa.
Matuzya aliwataja wachezaji waliokuwa nje kwa majeraha kuwa ni Nizar Khalfan, Shadrack Nsajigwa, Juma Abdul, Omega Seme, Jerryson Tegete pamoja na Stephen Mwasyika ambao wameanza mazoezi na wenzao.

Ligi hiyo itaendelea kesho, ambako Azam FC watashuka dimbani kuikabili Simba ambayo tayari imepoteza mwelekeo kutetea taji lake kwenye Uwanja wa Taifa.

MJADALA WA LWAKATARE NA UGAIDI WAWASHA MOTO BUNGENI.

 
DODOMA-TANZANIA,
MKURUGENZI wa Ulinzi na Usalama wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), anayekabiliwa na kesi ya ugaidi mahakamani, Wilfred Lwakatare, jana alilitikisa Bunge baada ya kuhusishwa katika mjadala.

Lwakatare alijadiliwa wakati wabunge walipokuwa wakichangia hotuba ya bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa mwaka wa fedha wa 2013/2014.
Aliyeanzisha mjadala huo, ni Mbunge wa Iramba Magharibi, Mwigulu Nchemba (CCM), ambaye alianza kwa kuwatuhumu viongozi wa Chadema, wamekuwa wakipanga kuua watu na wakati huo huo wakitaka wananchi wawape ridhaa ya kuongoza nchi.

Alisema pamoja na viongozi hao kuwa na tabia hiyo, wamekuwa wa kwanza kulalamika juu ya vitendo vyao na kwamba tabia hiyo ni sawa na mchawi ambaye akiroga mtu na kumuua, anakuwa wa kwanza kulia akionyesha uchungu alionao juu ya marehemu.

“Mheshimiwa Spika, kuna jambo ambalo limekuwa likiandikwa na kulalamikiwa na watu, kwamba ugaidi ugaidi. Katika jambo hili nawaomba Watanzania wasikilize kwa makini, kuna jambo lilitokea na jambo hili ni jambo la kigaidi, limeandikwa sana na kwa masikitiko linapotoshwa, yaani watu wanapotosha mpaka mambo yanayohusu maisha ya watu.

“Eti wanasema usalama wa taifa, mara wanasema polisi wanatesa watu, katika hili wala msihangaike na kwenye jambo hili hakuna polisi wala usalama wa taifa. Jambo la mkanda, aliyerekoki huo mkanda yuko tayari kusema kokote, aliyeniletea huo mkanda yuko tayari kusema kokote na mimi niko tayari kwenda kokote hata kama ni mbinguni.

“Chadema walipanga kuteka na kuua na huyu mwandishi walipanga kumuua eti wanadai picha ilitengenezwa, sasa kwa taarifa yenu hata pale alipokuwa anaongea, (akimaanisha Lwakatare), aliandika hata ile karatasi ninayo, ni hii hapa, fingerprint ni ya kwake, mwandiko ni wa kwake na vyote alivyokuwa anafanyia kazi vimepatikana na alisema atatoa ushahidi na mimi niko tayari kutoa ushahidi kokote iwe ni hapa na hata mbinguni nitakwenda,” alisema Mwigulu akionyesha karatasi hiyo na kuongeza.

“Eti Mbowe (Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe), anasema anayewasiliana na gaidi eti naye aunganishwe na ugaidi, hebu fikirieni, yule aliyekuwa akipanga njama ni Mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama wa Chadema, kama ni viongozi, amewasiliana na viongozi gani kama siyo wakubwa zake ambao wamemwagiza kufanya hayo tena?

“Jitihada zinazoonyeshwa ambazo ni za kumtetea mtu hata kabla hajafika mahakamani, inadhihirisha ule ulikuwa ni mpango wa chama.

“Kwa kauli hii, ambayo ameandika kiongozi wa upinzani, viongozi wanaowasiliana nao waunganishwe katika kesi ya ugaidi kuanzia leo wakamatwe na polisi, hapa simuoni kiongozi wa Kambi ya Upinzani, labda wameshamkamata,” alisema Mwigulu.

Katika mazungumzo yake, Mwigulu ambaye pia ni Naibu Katibu Mkuu wa CCM, alitaka Katibu Mkuu wa Chadema, Dk. Wilbrod Slaa, akamatwe kwa kuwa alihusika kumtetea Lwakatare.

Kwa mujibu wa Mwigulu, aliyekuwa akipanga njama za ugaidi huo ni mwanachama wa Chadema na kwamba fedha zilizotumika katika kufanikisha mpango huo, ni za chama hicho.

“Mnasubiri nini polisi, mtu ameshaomba kuunganishwa mwenyewe katika kesi?”

“Mkishapanga maovu mnawahi kwenda kutetea kama vile mchawi ambaye akishaua, anawahi kwenda kulia na kugalagala msibani. Mimi kwenye hili suala la mauaji, nawaomba Chadema mfanye vitu viwili, kwanza kimbieni haraka zaidi kwenye makanisa ama misikiti mliyokaribu nayo ili mkatubu kuwa mmepanga kuwauwa watu wasio na hatia.

“Baada ya kuomba toba, mrudi kutubu kwa wananchi, yaani mnataka uongozi halafu unawaza kuuwa watu, look at you,” alisema.

Wakati akiendelea kusema, Mbunge wa Mbulu, Mustafa Akunay (CHADEMA), aliomba utaratibu na kumlalamikia Mwigulu, kwamba anazungumzia masuala ya Lwakatare wakati akijua yako mahakamani.

Alipomaliza kusema hayo, Spika wa Bunge, Anne Makinda, alikubaliana naye na kuwataka wabunge waheshimu kanuni za Bunge. Hata hivyo hoja hiyo Mbunge wa Viti Maalum (Chadema), Pauline Gekul alisimama na kuomba mwongozo kwa kutumia Kanuni ya 68 (7).

Alipokuwa akizungumza, alionyesha kutoridhishwa na maelezo ya Spika kwa kuhoji kama wabunge wanatakiwa kufuata kanuni kwa nini Mwigulu alipokuwa akizungumzia masuala yaliyo mahakamani hakuzuiwa na badala yake aliachwa na kuendelea kusema hadi mwisho.

Hoja hiyo, ilimfanya Spika asimame tena na kusema wabunge wanatakiwa kufuata kanuni kwa kuwa hata Mbowe alipokuwa akiwasilisha maoni ya kambi yake juzi kuhusu bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu, kuna maneno yasiyofaa aliyasema, lakini akaachwa hadi mwisho.(MTANZANIA)

Friday, April 12, 2013

MIAKA 29 BAADA YA KIFO CHA EDWARD SOKOINE-HISTORIA,NUKUU NA PICHA

Hayati  Edward Moringe Sokoine


Edward Moringe Sokoine (1938 - 12 Aprili 1984) alikuwa Waziri Mkuu wa Tanzania kwa awamu mbili, tangu tarehe 13 Februari 1977 hadi 7 Novemba 1980, na tangu tarehe 24 Februari 1983 hadi kifo chake, alipofariki kutokana na ajali ya gari. 

Uongozi wake ulionekana kuwa wa mfano kwa jinsi alivyokuwa na uadilifu na kufuatilia utendaji kazi huku akikemea ulaji rushwa na ubadhirifu wa mali za umma. 

Sokoine alifariki kwa ajali ya gari wakati akitoka kwenye kikao cha bunge Dodoma kuelekea Dar es Salaam. Wengi wanashuku ajali hiyo kuwa ilipangwa, ingawa mpaka leo bado ni kiza kitupu.

Kifo chake kilileta majonzi makubwa kwa Watanzania wa kawaida ambao walikuwa wanamtarajia kuwatetea wanyonge na kuinua hali ya maisha yao. 
 
Mwili wa Edward Moringe Sokoine ulizikwa nyumbani kwao Monduli, mkoani Arusha.
Leo Tanzania inaazimisha miaka 29 tangu kufariki kwa ndugu Edward Moringe Sokoine (01/08/1938-12/04/1984)   Waziri Mkuu wa aina yake nchini Tanzania.Sokoine aliongoza katika kipindi ambacho nchi ilikuwa katika hali ngumu sana ya kiuchumi. 
Hayati Sokoine na Mwalimu Nyerere.
Zifuatazo ni nukuu muhimu za shujaa huyo kutoka katika Kitabu cha Edward Moringe Sokoine: Kiongozi wa Watu Aliyejitolea kilichoandikwa na Luteni Kanali Albert N. Kigadye mnamo mwaka 1984:


"Ole wake kiongozi mzembe na asiye na nidhamu nitakayemkuta: Kiongozi wa siasa hana usalama wa aina yoyote. Usalama wake ni kudra ya Mungu na Wananchi peke yake. Viongozi wazembe na wabadhirifu wahesabu siku zao. Labda tusiwajue. Hawa hatuna sababu ya kuwapa imani, kuwa tutawalinda kama vitendo vyao viovu" - Edward Moringe Sokoine, 26 Machi 1983

"Juu ya suala hili la mapato kutolingana na matumizi ni kwamba tungependa kupunguza uongezaji wa wataalam wasiohitajika katika Serikali na katika mashirika ya umma mpaka hapo hali yetu ya uchumi itakapokuwa katika hali nzuri" - Edward Moringe Sokoine, 23 Oktoba 1982
Gari la Hayati sokoine baada ya ajali.
"Serikali inasimamia bei, lakini Serikali yetu itakwenda mpaka itasimamia bei ya mhogo, dagaa na bei ya kila kitu? Haiwezekani, vitu vingine ni lazima vizalishwe kwa wingi ili bei yenyewe iweze kujirekebisha" - Edward Moringe Sokoine, 24 Septemba 1983

"Wajibu wa kila Mtanzania, kila familia na kila anayekula ni kujilisha mwenyewe. Si wajibu wa Taifa kumlisha mtu. Unaweza ukasaidiwa unapopatikana na janga. Lakini kama hakuna janga ni wajibu wa kila mtu aweze kujitosheleza kwa chakula na atoe ziada kwa Taifa" - Edward Moringe Sokoine, 4 Oktoba 1983

"Vijana leo wengi wana mali zaidi kuliko wazee waliofanya kazi miaka thelathini hadi arobaini. Lakini wanaitaka Serikali ndiyo iwaulize mali hiyo wameipata wapi. Hivi kwa nini mzazi asimuulize mwanae, 'mali hii umeipata wapi?'" - Edward Moringe Sokoine, 23 Oktoba 1983

"Katika nchi inayojali haki na usawa, majeshi hayana budi yawe ni chombo cha kulinda haki na maslahi ya walio wengi. Na kamwe hayaruhusiwi kuwa ni chombo cha wachache wenye kujali nafsi zao na kusahau maslahi ya walio wengi" - Edward Moringe Sokoine, 1Februari 1977

RAIS OMAR AL BASHIR KUZURU SUDAN KUSINI LEO.


JUBA-SUDAN KUSINI,Rais wa Sudan Omar Hassan Al Bashir anatarajiwa kuzuru nchini Sudan Kusini ijumaa hii na tayari maandalizi makubwa kwa ajili ya mapokezi yake yamekwishafanyika. Al Bashir anatarajiwa kukutana na mwenyeji wake Rais Salva Kiir na ziara hii itakuwa ni sehemu ya kumaliza mgogoro uliozuka baina ya pande hizo mbili.

Miongoni mwa mambo yatakayopewa kipaumbele katika mazungumzo ya viongozi hao ni suala la usalama ambalo limekuwa tete tangu nchi hizo zigawanyike mwezi Julai mwaka 2011.Muafaka kati ya viongozi hawa wawili unatajwa kuwa huenda ukawa chanzo cha kupunguza uhasama na hata kurahisisha utekelezaji wa makubaliano ya amani baina ya mataifa hayo.

Mpango wa Al Bashir kuzuru Juba uliwekwa wazi siku moja tu baada ya viongozi wa mataifa haya mawili ya Sudan kuafikiana kuanza upya biashara ya uzalishaji na usafirishaji wa mafuta.

Ziara ya Bashir mjini Juba itakuwa ni ya kwanza tangu kiongozi huyo alipohudhuria sherehe za uhuru julai 9 2011 kufuatia kura ya maoni iliyoamua Kusini ijitegemee baada ya miaka 22 ya machafuko.

CAG ABAINI UBADHILIFU MKUBWA SERIKALINI.


 

DODOMA-TANZANIA,
Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), ilitolewa jana ikiweka bayana madudu mbalimbali ya ubadhirifu mkubwa wa fedha za umma, udhaifu katika usimamizi wa mikataba na Serikali kushindwa kutoa fedha zilizoidhinishwa na Bunge kwa ajili ya miradi ya maendeleo.
Moja ya matatizo yaliyojitokeza ni Wizara ya Nishati na Madini kushindwa kukusanya nyongeza ya mrabaha wa madini baada ya kuongezwa kutoka asilimia tatu hadi nne.
Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kuwasilisha ripoti hiyo ya mwaka wa fedha unaoishia Juni 30, 2012, CAG Ludovick Utouh alisema pamoja na kuwapo mafanikio ya kimahesabu ukilinganisha na miaka iliyopita, bado kuna mambo ambayo yanatakiwa kufanyiwa kazi.
Alilishauri Bunge kuangalia upya suala la kuivunja Kamati ya Hesabu ya Mashirika ya Umma (POAC) na kuunganisha shughuli zake na Kamati ya Hesabu za Serikali Kuu (PAC) na mkakati wa ofisi kufanya ukaguzi wa misamaha ya kodi ambayo imeongezeka kuangalia uhalali wake.
Hata hivyo, Utouh alikataa katakata kuzungumzia deni la taifa ambalo pia limeongezeka akisema “amefanya hivyo makusudi”.
Bajeti na miradi ya maendeleo
Kwa mujibu wa CAG, imebainika kuwa kuna tatizo kubwa la Serikali kushindwa kutoa kwa halmashauri mbalimbali fedha za maendeleo kama zilivyopitishwa na Bunge.
Alisema Bunge lilipitisha vifungu vya fedha za maendeleo vyenye jumla ya Sh595,064,422,505 katika halmashauri 113, lakini fedha zilizopokewa ni Sh345,568,067,477 sawa na asilimia 42 tu, hivyo kufanya upungufu wa Sh249,496,355,027.
Licha ya fedha hizo kutokutolewa zote, kiwango kilichotolewa hakikutumika chote kutokana na kucheleweshwa. “Hadi mwishoni mwa mwaka, kulikuwa na baki ya fedha za miradi ya maendeleo kiasi cha Sh188,405,740,589 ambayo ni sawa na asilimia 55 ya fedha zilizotolewa na Serikali,” alisema Otouh na kuongeza: “Tunashauri bajeti iendane na shughuli zilizopangwa, kwa sasa utaratibu wa bajeti haujawa mzuri.”
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, hata fedha za Mfuko wa Maendeleo ya Jimbo zinazotolewa kwa wabunge hazikutumika zote. Sh2,561,882,820 zilizotengwa kwa ajili ya sampuli ya majimbo 69 zilibaki.
“Sababu ya kutokutumika ni ama halmashauri hazina utaratibu maalumu wa kutumia fedha hizo au Serikali kutoa fedha hizo mwishoni mwa mwaka,” alisema.
Udhaifu katika usimamizi wa mikataba ya madini
Katika ripoti hiyo, CAG alisema Wizara ya Nishati na Madini ilishindwa kukusanya Dola za Marekani 12,634,354 (sawa na Sh19,709,593,191) zilizotokana na ongezeko la mirabaha ya madini, baada ya mabadiliko ya Sheria ya Madini.
Katika iliyokuwa Wizara ya Miundombinu, ukaguzi huo umebaini kuwa madeni yake ya mwaka 2010/11 yanayofikia Sh253 bilioni yamelipwa kwa kutumia fedha zilizoidhinishwa kwa ajili ya ujenzi wa barabara mwaka uliofuata wa 2011/12.
Katika kipindi hicho, CAG alisema dhamana za Serikali za jumla ya Sh578.4 bilioni zilikuwa zimeisha muda wake na hivyo kuifanya Serikali ikiwa mdhamini kuwajibika kulipa deni hilo.
Vilevile, CAG ameona kuna kodi inayopotea kutoka sekta isiyo rasmi, hivyo kuishauri Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kuwatumia vizuri makatibu kata kuwatambua walipakodi kama vile wamiliki wa kumbi za harusi na mikutano.(MWANANCHI)

OBAMA AIONYA KOREA KASKAZINI KUHUSU KUISHAMBULIA MAREKANI





WASHINGTON DC-MAREKANI, Rais wa Marekani Barack Hussein Obama hatimaye amefungua kinywa chake na kuishauri Korea Kaskazini kuachana na mpango wake wa kutaka kuingia kwenye vita katika kipindi hiki wakati kukiwa na uvumi kuwa serikali ya Pyongyang inataka kushambulia Washington kwa makombora. 

 Obama ametoa kauli hiyo akiwa katika Ikulu yake maarufu kwa jina la White House na kueleza hakuna mtu yeyote ambaye anapenda kushuhudia Dunia inaingia kwenye mgogoro utakaochangia vita.
Aidha Rais Obama amesisitiza umuhimu wa serikali ya Korea Kaskazini kuheshimu sheria na taratibu kama inavyofanyika kwa nchi nyingine duniani ili kuepusha migogoro zaidi.
Korea Kaskazini pia haikukwepa kidole cha lawama kutoka kwa Mawaziri wa Mambo ya Nje kutoka nchi tajiri zaidi duniani maarufu kama G8 walipokutana nchini Uingereza.
Akizungumza na waandishi wa habari pembezoni mwa mkutano huo Waziri wa Mambo ya Nje wa Uingereza William Hague amesema endapo Pyongyang itafanya jaribio jingine la nyuklia hawatasita kuchukua hatua kali dhidi yake ikiwemo vikwazo vipya ambavyo vitaafikiwa katika baraza la usalama la umoja wa mataifa UNSC.
Hofu ya kutekelezwa kwa mashambulizi kutoka Korea Kaskazini kulenga Marekani na rafiki zake Japan na Korea Kusini imeendelea kuchanja mbuga licha ya makaripio mbalimbali kuzidi kutolewa kila uchao.

Thursday, April 11, 2013

OFISI YA WAZIRI MKUU KUTUMIA TRILIONI 4.2.

 

DODOMA-TANZANIA,
Waziri Mkuu, Mizengo Pinda ameliomba Bunge kuidhinisha Sh4.2 trilioni ambazo ni makadirio ya matumizi ya fedha kwa mwaka 2013/14 kwa ajili ya ofisi yake pamoja na Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa. Fedha hizo ni za matumizi ya kawaida na fedha za maendeleo za ndani na nje. Pinda alitoa ombi hilo alipokuwa akiwasilisha bungeni mjini Dodoma jana mapitio na mwelekeo wa kazi za Serikali na Makadirio ya Matumizi ya Fedha, Ofisi ya Waziri Mkuu na Ofisi ya Bunge kwa mwaka 2013/14. 

 Ameliomba Bunge liidhinishe Sh123.4 bilioni kwa ajili ya Mfuko wa Bunge, Sh114.5 bilioni kwa matumizi ya kawaida na Sh8.8 bilioni kwa ajili ya miradi ya maendeleo. Aliziombea ofisi za wakuu wa mikoa Sh193.8 bilioni na kati ya fedha hizo, Sh143.7 bilioni ni za matumizi ya kawaida na Sh50 bilioni za miradi ya maendeleo. “Halmashauri naziombea kiasi cha Sh3.6 trilioni na kati ya hizo, Sh2.9 trilioni ni za matumizi ya kawaida na Sh640.5 bilioni ni za miradi ya maendeleo,” alisema Pinda.  
 Katika hotuba hiyo, Pinda aligusia mambo mbalimbali ikiwa ni pamoja na uboreshaji wa daftari la wapigakura ambao unatarajiwa kukamilika Desemba mwaka huu kwa awamu ya kwanza. “Uboreshaji huo utawezesha kuchapishwa kwa daftari la wapigakura kwa ajili ya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa mwaka 2014 na Uchaguzi Mkuu mwaka 2015,” alisema Pinda. Pia alizungumzia suala la nchi kutoka katika mfumo wa analojia kwenda dijitali na kupigilia msumari akieleza kuwa Serikali itaendelea na mabadiliko hayo kama ilivyo sasa kuliko kusubiri na kujikuta iko nyuma na nje ya mstari. “Natoa wito kwa Watanzania wote kuyaona mabadiliko hayo kwa mtazamo chanya na kuyakubali kama hatua kubwa sana ya maendeleo ya teknolojia nchini,” alisema Pinda na kuongeza: “Katika mazingira ya sasa sisi kama taifa siyo vyema kubaki kama kisiwa wakati tumeunganishwa na mifumo ya teknolojia.” Pia alisema Serikali imekamilisha taratibu za kuanzisha halmashauri mpya 31 ili kuongeza huduma karibu na wananchi.(MWANANCHI)

Tuesday, April 9, 2013

BUNGE LA BAJETI KUANZA LEO.

 
DODOMA-TANZANIA, Mkutano wa 11 wa Bunge la Bajeti unaanza leo mjini Dodoma, huku kukiwa na mabadiliko kadhaa ya taratibu za uendeshaji wa Bunge.
Taarifa iliyotolewa jana na Mkurugenzi Msaidizi wa Bunge (Habari), Deogratius Egidio ilieleza kuwa Bunge litaanza vikao vyake leo na kukamilika Juni 28, mwaka huu.
Kutokana na mabadiliko hayo, leo asubuhi Bunge litapokea Azimio la Marekebisho ya Kanuni za Bunge ambalo linatarajia kuwasilishwa na Naibu Spika, Job Ndugai.
Egidio alisema katika mkutano huo, mambo kadhaa yanaonekana kubadilishwa ikizingatiwa na utaratibu uliozoeleka tangu mwanzo wa kusoma kwanza Bajeti ya Serikali na baadaye kumalizia na bejti za wizara mbalimbali.
Aliyataja mabadiliko hayo kuwa ni utaratibu mzima jinsi ya uwasilishaji bajeti za wizara, kwa mwaka huu itaanza Ofisi ya Waziri Mkuu ambayo itajadiliwa kwa siku tano. “Siku zote tumezoea kuona Bajeti ya Serikali ndiyo inayotangulia kuanza kuwasilisha bajeti yake, utaratibu huo umeonekana siyo mzuri kutokana na mapendekezo ya Mdhibiti na Mkaguzi wa Fedha za Serikali (CAG), hivyo tunaanza na wizara zingine ili fedha wawe mwisho,” alisema Egidio.
Hata hivyo, taarifa za zilizopatika kutoka ndani zinadai kanuni nyingi zinatarajia kubadilishwa na kwamba, iwapo zitapitishwa zitapunguza meno ya Bunge dhidi ya kusimamia Serikali.
Kwa mujibu wa mkurugenzi huyo, kesho itakuwa siku maalumu kwa Ofisi ya Waziri Mkuu kuwasilisha bajeti yake, ambayo itajumuisha wizara zote zilizo chini yake na inatarajia kujadiliwa kwa muda wa siku tano.
Mabadiliko mengine ni kuwasilishwa mezani kwa taarifa ya CAG kwa mwaka 2011/12 bila kujadiliwa na wabunge kama ilivyozoeleka.
Hata hivyo, Egidio hakueleza sababu za kutojadiliwa kwa ripoti hiyo, akisema hawezi kujua katika mikutano ya baadaye ya Bunge iwapo inaweza kupangiwa kujadiliwa.