Friday, April 4, 2014

Vikosi vya Marekani vyawasili Uganda kumsaka Kony

http://www.dw.de/image/0,,6478206_10,00.jpg

Kampala. Vikosi vya Marekani kwa ajili ya kumkabili kiongozi wa kundi la Lord Resistance Army (LRA) Joseph Kony vimewasili nchini Uganda huku vikiwa na vifaa vya kisasa zikiwamo ndege zenye uwezo wa kujaza mafuta angani.
Taarifa zimesema kuwa askari hao 150 waliwasili siku tatu zilizopita na kwamba sasa wanatazamiwa kuanzisha msako mkali katika maeneo ya mpakani mwa Uganda na Jamhuri ya Afrika ya Kati ambako kiongozi huyo anaaminika kujifisha.
Hivi karibuni Rais Barack Obama aliidhinisha kutumwa kwa vikosi hivyo kama sehemu ya kuunga mkono juhudi zilizoanzishwa na Umoja wa Afrika za kumsaka Kony ambaye pia anatakiwa na mahakama ya kimataifa ya uhalifu(ICC) kutokana na makosa ya uhalifu dhidi ya binadamu.
Askari hao wamewasili wakiwa na vifaa vya kisasa ikiwamo ndege aina ya CV-200 yenye uwezo wa kujaza mafuta ikiwa angani na kwamba mkakati wao wa kwanza ni kuelekea kwenye misitu ya Jamhuri ya Afrika ya Kati.
Ofisa habari katika ubalozi wa Marekani nchini Uganda Daniel Travis alithibitisha kuwasili kwa askari hao lakini hata hivyo hakuwa tayari kutoa maelezo zaidi.
“Hatuwezi kueleza zaidi kuhusiana mahali ambako vikosi hivyo vipo zaidi ya kusema kwamba vitakuwepo nchini kwa muda maalumu na hatutarajia kuona vinakuwepo zaidi ya muda ulioamuliwa,”alisema.
Vikosi hivyo vya Marekani vinatazamiwa kuongeza nguvu juhudi za kumsaka kiongozi huyo ambaye anatuhumiwa pia kwa kuwaandikisha askari watoto na kuhusika katika vitendo vya ubakaji.
Kwa muda mrefu vikosi vya Umoja wa Mataifa vimekuwa vikiendesha msako dhidi ya Kony bila mafanikio yoyote kutokana na kuhamisha mara kwa mara maficho yake. Vikosi hivyo vya Afrika vinaundwa na askari kutoka Uganda, Sudan Kusini, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo na Jamhuri ya Afrika ya Kati.

CHANZO:MWANANCHI

No comments:

Post a Comment