Sunday, November 4, 2012

IDADI YA VIFO KUTOKANA NA KIMBUNGA MAREKANI YAFIKIA 90


Madhara ambayo yamechangiwa na Kimbunga Sandy kilichopiga Jiji la New York nchini Marekani
MAREKANI, Idadi ya vifo vilivyosababishwa na kimbunga kikali cha Sandy ambacho kimepiga nchi ya Marekani hasa majiji ya New York na New Jersey imeongezeka na sasa watu wanaokadiriwa kufikia tisini wanatajwa kupoteza maisha. Kimbunga Sandy ambacho kinatajwa kuwa kikali zaidi kupiga nchi ya Marekani katika kipindi cha miaka mitatu kimeendelea kucha madhara makubwa ikiwemo ukosefu wa huduma ya umeme kwa wananchi.

Mamlaka nchini Marekani zimethibitisha watu milioni nne na laki tano kutoka majimbo kumi na mawili nchini humo wameendelea kukosa huduma ya umeme huku tatizo la upatikanaji wa mafuta nalo likijitokeza.
Kimbunga Sandy ambacho kimepiga zaidi eneo la Mashariki mwa Marekani kimesababisha hasara ya dola bilioni hamsini na kwa sasa serikali inaendelea na juhudi za kusafisha maeneo ambayo yamekubwa na madhara hayo.
Idadi ya vifo inatajwa huenda ikaongezeka kutokana na kila waokoaji wanapofika wanakutana na miili ya watu ambao wamepoteza maisha kutokana na kimbunga Sandys ambacho kilianzia Caribbean.

Kikosi Maalum ambacho kinafanya msako wa kutafuta watu waliopoteza maisha wameendelea kuahidi zoezi hilo litakuwa limekamilika haraka iwezekanavyo ili kujua idadi kamili ya watu waliopoteza maisha.

Takwimu zinaonesha watu wengi wamepoteza maisha katika Jiji la New York ambapo Mamlaka za Jiji hilo zinaeleza watu thelathini na wanane wamepoteza maisha huku wengine kadhaa wakiwa hawajulikani walipo.
Harakati hizi zinaendelea huku baadhi ya huduma zikiwa zimeanza kurejea kama ilivyokuwa awali huku njia za reli za chini ya ardhi nazo zikifunguliwa kwa mara ya kwanza pamoja na safari za ndege kuendelea kama kawaida.
Serikali nayo imeahidi kufika siku ya jumamosi huduma ya umeme itakuwa imerejeshwa katika maeneo yote ambayo huduma hiyo ilitoweka kipind ambacho Kimbunga Sandy kilisababisha madhara(chanzo RFI)

No comments:

Post a Comment